Mnyika, Msigwa walipuka bungeni madai ya makada wa Chadema kubambikiwa kesi na Polisi



Wabunge wa Chadema, John Mnyika kutoka Kibamba na Peter Msigwa wa Iringa vijijini leo Juni 5, 2018 wameibana serikali bungeni kuhusu madai ya wananchi hasa viongozi na makada wa chama hicho kubambikiwa kesi na askari polisi.

Akizungumza bungeni Msigwa alidai kuwa, kuna tabia iliyoibuliwa na baadhi ya askari polisi ya kuwabambikizia kesi viongozi na makada wa vyama vya upinzani hasa wa Chadema, na kwamba  huwalazimisha kuhamia chama tawala ili wasibambikiwe kesi.   

“Tabia ya polisi kubambikizia kesi, mimi ni muhanga wa kubambikiziwa kesi, RCO wa Iringa anatabia ya kulazimisha wananchama wa Chadema kuhamia CCM ili wasibambikiziwe kesi,” alidai Msigwa.

Akijibu swali Msigwa, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Eng. Hamad Massauni “madai ya Msigwa amekuwa anayatoa mara kwa mara bungeni na nilimuomba alete uthibitisho lakini haleti, kwa taarifa zilizopo hadi sasa hakuna askari polisi aliyekutwa anafanya matendo hayo kinyume na sheria.”

Akiuliza swali la Mbunge wa Tarime Vijijini John Heche, Mnyika alidai kwamba kuna kesi nyingi wanazobambikiziwa baadhi ya wananchi hasa kesi za wizi na mauaji, na kuhoji kuwa kwa nini serikali isiwasaidie wahanga wa vitendo hivyo kwa kuwapatia msaada wa kisheria.

Pia, Mnyika aliitaka serikali kuruhusu Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora iende kufanya uchunguzi katika gereza la Tarime kubaini watuhumiwa waliobambikiziwa kesi, vile vile alihoji serikali itaanza lini kulipa fidia watu wanaobambikiziwa kesi ili tabia hiyo ikome.

Akijibu swali la Heche kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, Naibu Waziri wa Kazi, Vijana na Ajira, Mhe. Antony Mavunde amesema “Utaratibu wa kimahakama uko wazi, inapotokea mtu ameshtakiwa mahakamani, na ikagundulika amebabmbikiziwa kesi inamtaka afungue kesi za madai, utaratibu upo na watu wafuate sheria.”
                           



Post a Comment

Previous Post Next Post