Ufafanuzi wa ACT juu ya sintofahamu kuhusu ushirikiano wake na Chadema Buyungu


Chama cha ACT-Wazalendo kimetoa ufafanuzi wa sintofahamu kuhusu ushirikiano wake na Chadema katika kusimamisha mgombea mmoja kwenye uchaguzi mdogo wa Jimbo la Buyungu unaotarajiwa kuitishwa baada ya mbunge wake, Mwalimu Kasuku Bilago kufariki dunia.

Ufafanuzi huo umetolewa na Kiongozi wa Chama wa ACT, Zitto Kabwe ambapo amesema uamuzi huo ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya mwelekeo wa chama hicho yaliyoafikiwa na kikao chake cha mwezi Januari mwaka huu.

“Chama cha ACT Wazalendo Katika Kikao chake cha Januari Mwaka 2018 kiliazimia katika mwelekeo wa Chama Mwaka 2018 kuwa ni Muhimu kujenga mashirikiano na vyama vingine na makundi mengine ya kijamii. Mwelekeo huo umewekwa hapa pia. Tunataka kujenga a DEMOCRATIC FRONT kwa kuhusisha wana Demokrasia nchini kwa madhumuni ya kutetea, kuimarisha na kulinda demokrasia yetu ya vyama vingi na kujenga Uchumi shirikishi wa Wananchi ( inclusive economy),” amesema Zitto kupitia taarifa yake kwa umma aliyoitoa leo.
                       

Zitto amefafanua kuwa “Mnamo tarehe 30/ 5/2018 Viongozi wa Vyama 2 vya upinzani nchini Kabwe Zuberi Ruyagwa Zitto na Freeman Aikael Mbowe walitamka dhamira ya kushirikiana kwa kuanzia kuweka mgombea mmoja wa ubunge Jimbo la Buyungu Mkoa wa Kigoma na hatimaye nchi nzima. Makubaliano haya ambayo yanarejewa kama MAKUBALIANO YA KAKONKO hatimaye yatafikishwa kwenye vikao vya Vyama vya ACT Wazalendo na CHADEMA ili kupata baraka za wanachama.”

Post a Comment

Previous Post Next Post