Serikali yatangaza neema matumizi ya gesi majumbani, wananchi kupewa mitungi bure


Serikali imetangaza mikakati yake minne katika kuboresha matumizi ya gesi kwa wananchi, ikiwemo kuendeleza usambazaji wa mabomba ya gesi majumbani, pamoja na kuanzisha mfumo wa wananchi kupatiwa mitungi iliyojaa gesi bure, kisha kulipia gharama kadri wanavyotumia.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano na Mazingira, January Makamba katika sherehe ya ufunguzi wa wiki ya misitu inayotarajiwa kuisha Juni 5, 2018 ambayo ni siku ya mazingira duniani,
iliyofanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Salaam.

Waziri Makamba amesema serikali iko katika mazungumzo na wauzaji wa mitungi ya gesi nchini ili waanzishe mfumo huo utakaosaidia wananchi wengi hasa wa kipato cha chini kutumia nishati hiyo na kupunguza uharibifu wa mazingira.


“Matumaini mengine ni gesi ya mitungi, mimi nimekuwa mlezi wa wauzaji wa gesi tumewaomba waunde chama ili waweze kuleta mambo yao serikalini ili kusaidia bei ya uuzaji mitungi ya gesi ishuke gharama. Kuna ubunifu katika eneo hili,” amesema  Waziri Makamba na kuongeza.


“Moja ya sababu iliyokuwa inasababisha watu wasitumie mitungi ni gharama ya mitungi, lakini sasa hivi kuna kampuni inajaribisha teknolojia na sisi tumewahimiza, ubunifu sababu sasa itawezekana katika mtungi ule wa laki moja kuna mita ambapo unaweza kuingiza kwa kutumia M-pesa kununua gesi, atapewa mtungi umejaa gesi lakini analipa fedha kwa kadri anavyotumia kwa M-pesa katika mita aliyolipa pale.”

Post a Comment

Previous Post Next Post