Alichozungumza Dkt. Bashiru baada ya kukabidhiwa ofisi


Baada ya kukabidhiwa rasmi ofisi, Katibu Mkuu mpya wa CCM, Dkt. Bashiru Ally amesema kazi aliyopewa na Halmashauri kuu ya chama hicho ni kufanya siasa ya mezani na si ya majukwaani, na kwamba atazungumzia na au kuchambua masuala yanayoamuliwa na kamati hiyo.

Dkt. Bashiru amesema maneno hayo mbele ya wanahabari baada ya kukamilika kwa shughuli ya makabidhiano ya ofisi iliyofanyika leo Mei 31, 2018 katika ofisi ndogo ya CCM iliyoko Lumumba jijini Dar es Salaam. Amekabidhiwa ofisi na Abdulrahman Kinana aliyejiuzulu wadhifa huo.

“Kazi niliyopewa si ya jukwaa, si siasa ya majukwaani, siasa ya majukwani ni  ya mwenyekiti wa chama akisaidiwa na makamu wake wawili, kule mikoani tuna wenyeviti wa vyama, wabunge na madiwani. Nazungumza kama katibu mkuu nikiwa msemaji wa chama na msimamo wa vikao vya halmashauri kuu ambacho ndio chombo kilichoniteua na chenye uwezo wa kunifukuza, siwezi kuchambua yale yasiyoamuliwa kwenye kikao,” amesema Dkt. Bashiru.


Dkt. Bashiru ameongeza kuwa “Ni marufuku kwa watendaji kufanya kazi ya wanasiasa, kazi ya kupiga siasa safi ni ya wale waliochaguliwa kwa muda wa miaka mitano, kama mtendaji hamtaniona kwenye majukwaa sababu wapo waliopewa dhamana ya kusema kwenye majukwaa, kazi yangu mimi ni kutoa taarifa kwenye vikao, kusimamaia maelekezo ya chama hayo si masuala ya jukwaani masuala ya mezani.”

Post a Comment

Previous Post Next Post