CUF kwaibuka mapya, Maalim Seif amwandikia barua Jaji Mutungi


Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi-CUF, Maalim Seif Shariff Hamad amemwandikia barua Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, Jaji Francis Mutungi  kuhusu mkutano mkuu wa chama hicho uliotishwa na Mwenyekiti wake anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vyama vya siasa, Profesa Ibrahim Lipumba.

Taarifa hiyo imetolewa asubuhi ya leo kwa umma na Naibu Mkurugenzi wa Habari, Mawasiliano na Umma, Mbarala Maharagande.


Sehemu ya taarifa hiyo inaeleza kuwa, mkutano huo unatarajiwa kufanyika Juni 17, 2018 mkoani Singida ambapo Jaji Mutungi anatarajiwa kuhudhuria katika mkutano huo. Barua ya Maalim Seif iko hapo chini.
THE CIVIC UNITED FRONT (CUF- Chama Cha Wananchi)

Office of the Secretary General,   Party Headquarters, P.O.  Box 3637, Zanzibar, Tanzania

Our Ref:  CUF/HQ/AKM/003/018/09                         Date: 21 Mei, 2018

 Mhe. Jaji Francis Mutungi
Msajili wa Vyama vya Siasa
Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa
Kivukoni Ilala CBD
1 Shaaban Robert Street
P.O. Box 63010
DAR ES SALAAM


KUH: KUENDELEA KUTUMIA VIBAYA DHAMANA ZAKO NA OFISI UNAYOIONGOZA KUENDESHA NJAMA ZA HUJUMA DHIDI YA THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – CHAMA CHA WANANCHI)

Tafadhali husika na mada iliopo hapo juu.

THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – Chama Cha Wananchi) ambacho ni chama cha siasa halali ndani ya Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania, kimepata taarifa za uhakika kwamba katika kuendeleza njama zako ovu dhidi ya chama chetu na ili kuvuruga mwenendo wa kesi zinazoendelea katika Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusiana na mambo kadhaa yanayokihusu chama chetu na ambayo pia yanakuhusisha wewe na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa unayoiongoza, umemuelekeza Ibrahim Haruna Lipumba na genge lake waandae Mkutano Mkuu batili wa Taifa (fake National Conference) hapo tarehe 17 Juni, 2018 kwa madhumuni ya kuwaondoa viongozi halali waliopo wa Chama na nafasi zao kuwaweka viongozi batili.

Taarifa hizo za uhakika tulizozipokea zinasema kwamba umewaelekeza kwa sababu za kimkakati Mkutano Mkuu huo batili uwe wa kushtukiza na usifanywe Dar es Salaam wala Zanzibar na badala yake wafikirie Singida, Mwanza, Tabora au Morogoro.

Kwa malengo ya kufanikisha njama hizo chafu na za kihuni, taarifa zimetuthibitishia kwamba wewe kupitia mwendelezo wa kuitumia kwako vibaya dhamana uliyopewa na pia kuitumia vibaya Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa, umewahakikishia kwamba utawapatia ‘mkopo’ wa shilingi milioni 600/- mwisho wa mwezi huu wa Mei, na kwamba tarehe 15 Juni fedha hizo zitaachiwa kwenda akaunti ya Temeke (ambayo ndiyo mmekuwa mkiitumia kufanyia uhalifu wa kuhamisha fedha za ruzuku ya CUF kuwapa Lipumba na genge lake kinyume na sheria) na zitachukuliwa zote kwa pamoja kama fedha taslimu (cash) kwenda sehemu itakayoamuliwa kufanyia Mkutano Mkuu huo batili.

Tunazo taarifa kwamba katika maelekezo yako hayo uliyowapa Lipumba na genge lake umewaambia wasishughulike na masharti na matakwa ya Katiba ya THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – Chama Cha Wananchi) ya mwaka 1992 (Toleo la 2014) katika kufanya Mkutano Mkuu huo batili kwani wewe utautambua na kuidhinisha maamuzi yake.

Kwa kuwa wewe ndiye mwenye kuhifadhi katiba za vyama vyote vya siasa, nina hakika unajua kwamba kipindi cha uongozi wa Chama ndani ya CUF ni miaka mitano. Ibara ya 113 ya Katiba ya CUF ya 1992 (Toleo la 2014) inaeleza:

“113. Isipokuwa pale ambapo Katiba imeeleza vinginevyo masharti ya    kuchaguliwa kwa kiongozi na kipindi cha uongozi kitakuwa kama hivi:-

(1)            Kipindi cha uongozi wa Chama kitakuwa miaka mitano (5) kwa ngazi zote isipokuwa kama kiongozi huyo ameshindwa kazi aliyopewa.

(2)            Iwapo kipindi cha uongozi kimemalizika na kuna sababu za msingi na za kitaifa kusababisha kwamba uchaguzi wa viongozi hao hauwezi kufanyika basi muda wa uongozi utaendelea kwa kipindi kingine cha miezi isiyozidi sita (6) na baada ya hapo ni lazima uchaguzi mpya uitishwe.”

Uongozi wa Chama uliopo ulichaguliwa kupitia Mkutano Mkuu wa Taifa uliofanyika mwezi Juni, 2014 na ambao taarifa za kumbukumbu zake zote unazo kwani ziliwasilishwa kwako rasmi kama Sheria ya Vyama vya Siasa inavyoelekeza. Ndiyo kusema kipindi cha uongozi uliopo kinamalizika Juni 2019. Kutaka kwako kulazimisha uchaguzi batili na haramu kupitia Lipumba na genge lake kipindi hiki ni kukiuka masharti ya Katiba ya CUF ambayo wewe ukiwa mwenye dhamana ya kutunza Katiba za Vyama unapaswa kuilinda na kuitetea.

Isitoshe kutokana na kesi zilizopo Mahakamani ambazo zinahusu kupata uhalali wa vyombo muhimu vya Chama na maamuzi yake, hiyo inatosha, ikiwa patakuwa na haja hiyo, kuwa sababu iliyoelezwa katika Ibara ya 113(2) tuliyoinukuu hapo juu ya kusogeza mbele Uchaguzi wa Chama ndani ya Chama kwa kipindi kisichozidi miezi sita (6).

Mbali ya hayo, kwa mujibu wa Ibara ya 63(2)(iv) na (v), na Ibara ya 78(1)(l) na (m), utaratibu wa kuwapata wajumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wakati wake ukifika unaujua kwamba ni kupitia uchaguzi unaofanywa na ngazi ya uwakilishi ambayo ni Mikutano Mikuu ya Wilaya za Tanzania Bara na Zanzibar. Wajumbe wengine wa Mkutano Mkuu wa Taifa wanatajwa katika Ibara ya 78(1)(a) –(t). Wajumbe wa Mikutano Mikuu ya Wilaya nao wanatokana na Kata kwa Tanzania Bara na Majimbo kwa Zanzibar [Ibara ya 62(2)(a)-(p)] ambapo Wajumbe wa Mikutano Mikuu ya Kata [Ibara ya 31(2)(a)-(h)] na Majimbo [Ibara ya 45(2)(a)-(h)] nao wanatokana na Mikutano Mikuu ya Matawi inayowajumuisha wanachama wote waliomo kwenye matawi husika [Ibara ya 17(2)].

Masharti haya ya Katiba ya CUF ya 1992 (Toleo la 2014) unayafahamu vyema maana yamekuwa yakisimamiwa na Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwa miaka yote kabla ya wewe kukubali kujishusha hadhi na kutumika kuyavuruga kwa maslahi yako na wale unaowatumikia.

Tunajua kuwa makubaliano yenu (kati yako na Lipumba na genge lake) kulingana na maelekezo yako ni kwamba genge hilo waonekane tu wamesambaza fomu za uchaguzi wa Chama ndani ya Chama hata bila ya kuzingatia na kufuata maelekezo na masharti ya Katiba ya Chama na Kanuni za Uchaguzi wa Chama ndani ya Chama. Umewaelekeza kuwapa watu wowote, hata kama si wanachama wa CUF, fomu hizo ili wazijaze na kisha kuwapanga katika nafasi mbali mbali za uongozi wa ndani ya Chama ikiwemo ujumbe batili wa Mkutano Mkuu huo batili (ambalo ndilo lengo kuu) hata kama hakutafanyika uchaguzi.

Maelekezo hayo umewapa baada ya kushindwa kwenu na njama zenu za awali za kuwarubuni viongozi wa Chama halali na wajumbe halali wa Mkutano Mkuu wa Taifa kutoka kwenye Wilaya za Tanzania Bara na Zanzibar ili wafanye kile mnachokitaka ambapo viongozi na wajumbe hao halali walikataa kutumika kukivuruga na kukihujumu chama chao wenyewe walichokijenga kwa jasho lao na damu zao kupitia mateso makubwa waliyopitishwa na dola tokea 1992 hadi hii leo.


Katika njama zenu hizo chafu na za kihuni, umewahakikishia Lipumba na genge lake kwamba wakifanikisha maelekezo uliyowapa, wewe utautambua uongozi batili utakaopachikwa na baada ya hapo vyombo vya dola vitakamilisha kazi iliyobaki ya kuzidhibiti ofisi zote za CUF nchi nzima na kuzikabidhi kwa Lipumba na genge lake. Umewaambia baada ya hapo, hata viongozi halali wa Chama tukifungua kesi kupinga uhuni huo mnaouandaa itachukua mwaka mwingine mzima na hivyo kufanikisha malengo yenu maovu.

Hivi ndivyo mtu mwenye nafasi ya Jaji wa Mahakama Kuu ulivyoamua kujidhalilisha alimradi tu unafanikisha matakwa yako binafsi na ya wale waliokutuma, lengo likiwa ni kuviua vyama makini vya siasa vinavyotoa ushindani wa kweli dhidi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM). Imeamuliwa kuihujumu CUF mara tu baada ya kile kilichoitwa uchaguzi wa marudio Zanzibar kutokana na CUF kuishinda vibaya CCM katika nafasi ya Urais wa Zanzibar, Ujumbe wa Baraza la Wawakilishi na Madiwani katika uchaguzi mkuu wa Zanzibar wa tarehe 25 Oktoba, 2015. Imeamuliwa pia kuihujumu CUF kwa sababu ya kuwa mshirika muhimu ndani ya Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ambao uliipa wakati mgumu CCM katika uchaguzi mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa tarehe 25 Oktoba, 2015 kuliko wakati mwengine wowote tokea ulipoanzishwa tena mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992. Lengo ni kuwa na CUF kama chama kibaraka (puppet party) kitakachoongozwa na vibaraka wa CCM ili kukisaidia watawala hao wabaki mdarakani.

Najua hii si mara ya kwanza kukuandikia na kukueleza kuhusu ushiriki wako binafsi na wa ofisi ya umma unayoiongoza, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa,   katika kupanga, kuendesha na kuongoza hujuma dhidi ya chama chetu, THE CIVIC UNITED FRONT (CUF – Chama Cha Wananchi). Sitowacha kufanya hivi nikitambua kama unavyotambua wewe kwamba kufanya hivi ni kuweka kumbukumbu za haya unayotenda. Kwa upande wetu sisi tutahakikisha tunakilinda Chama chetu na tunailinda demokrasia ndani ya nchi yetu na tunaulinda mfumo wa vyama vingi vya siasa hapa nchini.

                                                                    HAKI SAWA KWA WOTE


SEIF SHARIF HAMAD
KATIBU MKUU



Nakala kwa:

§  Mhe. Jenesta Mhagama (MB),
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu,
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
DODOMA.


§  Mhe. Jaji Mkuu,
Mahakama ya Rufani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
DAR ES SALAAM.


§  Mhe. Jaji Kiongozi,
Mahakama Kuu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
DAR ES SALAAM.


§  Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP),
Jamhuri ya Muuungano wa Tanzania,
DAR ES SALAAM. 

Post a Comment

Previous Post Next Post