Mitandao ya kijamii yakosesha usingizi viongozi wa Afrika Mashariki


Nchi za Afrika Mashariki hivi karibuni zimechachamaa kufanya mabadiliko na kutekeleza sheria za mtandaoni, huku sababu kuu ya msukumo huo ikiwa ni kudhibiti uhalifu wa mtandaoni ikiwemo usambazaji wa taarifa za uongo na uchochezi.

Leo Juni 1, 2018 nchi ya Rwanda imeungana na nchi nyingine za ukanda huo kufanya maboresho ya sheria za mtandaoni ambapo bunge lake lilipitisha sheria ya uhalifu wa mtandaoni yenye nia ya kusaidia sekta za kiserikali na binafsi kudhibiti uhalifu huo kwa kulinda taarifa za serikali na binafsi.

Hatua hiyo ya Rwanda pia ilifanywa na Uganda ambapo Rais wake Yoweri Museven hivi karibuni alipendekeza Waganda wanaotumia mitandao ya kijamii hasa wa Facebook na WhatsApp watozwe kodi ili kukabiliana na tatizo la usambazaji habari za uongo, lakini mapendekezo hayo yamesitishwa baada ya wizara ya fedha nchini humo kutaka kushauriana na wadau kuhusu uidhinishwaji wa mpango huo.

Nchini Kenya, Rais Uhuru Kenyatta hivi karibuni aliidhinisha mswada wa uhalifu wa kompyuta na mtandaoni wa 2018 kuwa sheria. Ambapo sheria hiyo itatoa adhabu ya Sh. Milioni 5 au kifungo cha miaka miwili jela na au adhabu zote mbili kwa atakayepatikana na kosa la usambazaji wa taarifa za uongo.

Wakati hayo yakijiri Kenya, Uganda na Rwanda, kwa upande wa Tanzania kuna sheria ya makosa ya mtandaoni ya mwaka 2015 ambayo inatumika kwa ajili ya kudhibiti vitendo vya uhalifu mtandaoni.



Post a Comment

Previous Post Next Post