Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema amefikishwa mahakamani
tena mchana wa leo, April 27, 2018 na kusomewa kosa moja la kuamsha hisia kwa
njia isiyohalali kinyume cha sheria.
Hii ni baada ya Lema kuachiwa huru mapema leo na Mahakama ya
wilaya (Sekei) baada ya upande wa Jamhuri kuondoa mashtaka yaliyokuwa
yakimkabili baada ya serikali kudai haina nia ya kuendea.
Hata hivyo baada ya kutoka mahakamani alipokeawito kutoka kwa
mkuu wa upelelezi wa polisi mkoa wa Arusha akitakiwa kufika katika mahakama ya
hakimu mkazi, Arusha ambapo alisomewa shtaka hilo.
Mbele ya hakimu, Nelson Baro mwendesha mashtaka wa serikali,
Eliainenyi Njiro aliieleza mahakama hiyo kwamba, mshtakiwa Lema, mnamo tarehe
22 Oktoba mwaka 2016 katika eneo la kambi ya Fisi ndani ya Jiji la Arusha
alitamka maneno yenye kuamsha hisia isiyo halali.
Maneno hayo ni "Rais Magufuli akiendelea na tabia ya
kudhalilisha demokrasia na uongozi wa upinzani iko siku taifa litaingia kwenye
umwagaji wa damu.
“Rais yeyote ambaye haheshimu mipaka ya sheria, mipaka ya
Katiba, Rais huyo ataingiza taifa katika
majanga na umwagaji damu, watu watajaa vifua, wakiamua kulipuka polisi hawa
wala jeshi halitaweza kudhibiti uhalifu utakaojitokeza.”
Hata hivyo mshtakiwa Lema alikana shtaka na upande wa
jamhuri ulidai hauna pingamizi la dhamana, jambo ambalo mshtakiwa alikidhi
sharti la dhamana kwa mdhamini mmoja aliyesaini bondi ya shilingi za kitanzania
milioni tano.
Hakimu Baro aliahirisha shauri hilo hadi Mei 30 mwaka huu
itakapokuja kwa ajili ya kutajwa baada ya upande wa Jamhuri kudai upelelezi bado
haujakamilika.
Kesi hiyo ni namba 132 ya mwaka 2018.
