Karia aipongeza Yanga


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)   Wallace Karia  ameipongeza klabu ya Yanga baada kufanikiwa kutinga katika hatua ya Makundi Kombe la Shirikisho Barani Afrika.

Yanga wamefuzu  katika hatua  hiyo kwa ushindi wa jumla wa  mabao 2-1 baada ya  mchezo wa awali kushinda kwa  mabao 2-0 kabla ya kufungwa bao 1-0 walipokuwa ugenini dhidi ya Welayta Dicha ya Ethiopia.

Rais wa TFF, Karia ametoa pongezi hizo kwa niaba ya TFF baada ya  Yanga kufanikiwa kutinga katika hatua hiyo na ikiwa ni timu pekee inayoiwakilisha Tanzania katika michuano hiyo, baada ya wekundu wa msimbazi Simba kuondoshwa katika michuano hiyo.

Yanga wameingia nchini usiku wa jana,wakitokea Ethiopia na kulakiwa na baadhi ya washabiki waliojitokeza kuwapokea, kesho Yanga watafunga safari kuelekea Mbeya kwa ajili ya mchezo wao wa Ligi Kuu Bara, dhidi ya wenyeji wao Mbeya City, mchezo utakaorindimwa katika uwanja wa Sokoine mijini Mbeya.

Droo ya  michuano hiyo itafanyika kesho Aprili 21, katika makao makuu ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) Cairo, nchini Misri kuanzia majira ya Saa 8:00 mchana.

Na usiku wa leo meneja wa Yanga, Hafidh Kido, anatarajia kwenda nchini Misri kuiwakilisha Yanga katika droo hiyo.


Post a Comment

Previous Post Next Post